Breaking News

RAIS KAGAME AWATOA JELA MWANAMUZIKI KIZITO MIHIGO NA MPINZANI WAKE VICTOIRE INGABIRE UMUHOZA

RAIS wa Rwanda, Paul Kagame amewapa msamaha wa kifungo cha jela, jumla ya wafungwa 2,140 miongoni mwao ni mwanamuziki mashuhuri Kizito Mihigo na mwanasiasa wa upinzani mwenye msimamo mkali mwana mama Victoire Ingabire Umuhoza. Kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini Rwanda, Msamaha huo wa Rais umetangazwa na Wizara ya Sheria Septemba 15, 2018 na tayari watu hao wametolewa magerezani.

Wakati Kizito Mihigo alikuwa, akitumikia kifungo cha miaka 10 jela baada ya kukutwa na hatia ya kupanga njama za kumuua Rais Paul Kagame na viongozi wengine wa juu wa serikali, Mwanasiasa Victoire Ingabire Umuhoza yeye alikuwa anatumikia kifungo cha miaka 15 jela baada ya kukutwa na hatia ya uchochezi na uasi dhidi ya serikali ya Rais Paul Kagame na pia kuunda vikundi vyenye silaha kwa lengo la kuhatarisha usalama wa nchi. Mwanasiasa huyo alikuwa kifungoni tangu mwaka 2010, huku Mwanamuziki huyo nyota nchini Rwanda, yeye alikuwa gerezani tangu mwaka 2015.

No comments